MZUNGUKO WA UKANUSHI WA JESPERSEN KATIKA LUGHA YA KISWAHILI

Authors

  • Issaya Lupogo Author

DOI:

https://doi.org/10.2023/hn35p166

Abstract

Mzunguko wa Ukanushi wa Jespersen ni mfuatano wa michakato katika Isimu Historia ambao huelezea maendeleo ya kihistoria ya ukanushi katika lugha mbalimbali unaojenga mzunguko. Kwa kuwa Mzunguko wa Ukanushi wa Jespersen (MUJ) bado haujatazamwa katika lugha ya Kiswahili, makala haya yanakusudia kuziba pengo hilo. Makala haya ni matokeo ya uchambuzi wa mapitio ya maandiko mbalimbali yahusuyo ukanushi. Baadhi ya mifano ya tungo za ukanushi ni kutoka kwa mwandishi kutokana na tajiriba na utaalamu alionao katika isimu ya lugha ya Kiswahili na Kiingereza. Tajiriba hii inatokana na ufundishaji wa kozi za mofolojia na fonolojia kwa takribani miaka sita. Moja ya mapitio ya msingi ni Ashton (1944) japo yeye na wengine waliomfuata hawakugusia suala la MUJ. Makala haya yamebainisha kuwa katika lugha ya Kiswahili, MUJ ni vigumu kubainishwa kihistoria/kidaikronia kama ilivyobainishwa na Jespersen. Akitumia mfano wa lugha ya Kifaransa, kabla ya lugha hiyo haijasanifishwa kulikuwa na umbo moja la ukanushi ne lililokuwa likijitokeza kabla ya kitenzi, baada ya lugha hiyo kusanifishwa; umbo lingne la ukanushi pas liliongezeka mwishoni mwa kitenzi na baadaye Kifaransa cha mitaani kiliibuka huku kikipuuza kutumia kikanushi ne, hivyo, kurudi tena katika mfumo wa ukanushi wa mwanzo wa tungo kuwa na kikanushi kimoja. Mtiririko huu ulionekana kujenga hali ya mzunguko/uduara. Makala haya yamebainisha kwamba suala hilo katika Kiswahili hujitokeza kisinkronia kwa kuutazama ukanushi kwa jinsi ulivyo kwa wakati wa sasa (kipindi hiki cha miaka ya 2000) katika Kiswahili. MUJ katika Kiswahili hujitokeza katika misingi kwamba baadhi ya vitenzi vina umbo moja la ukanushi wakati vitenzi vingine vina maumbo mawili. Kimantiki, tungo hizo zenye maumbo mawili ya ukanushi zinaonesha kuwa na dhana ya maana ya ukanushi moja na siyo mbili ndani ya kitenzi kimoja. Kwa hivyo, vinaleta hali ya mzunguko kwa maana ya kwamba kumekuwa na ongezeko la kikanushi cha pili lakini dhana ya maana ya ukanushi imerudi kuwa moja sawa na vitenzi vyenye kikanushi kimoja.

Downloads

Download data is not yet available.

Published

2025-01-22

How to Cite

Lupogo, I. (2025). MZUNGUKO WA UKANUSHI WA JESPERSEN KATIKA LUGHA YA KISWAHILI. JARIDA LA CHAUKIDU, 150-160. https://doi.org/10.2023/hn35p166